Monday, August 19, 2013

Wafuasi wa Ponda wapiga kambi Segerea



Ofisa Habari wa Magereza, Deodatus Kizinja alisema kisheria ni watu wawili tu kwa mwezi wanaoruhusiwa kumwona mahabusu mmoja.
Dar es Salaam. Wafuasi wa Kiongozi wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Issa Ponda wamepiga kambi katika Gereza la Segerea, Dar es Salaam wakitaka kumwona bila mafanikio.
Wakizungumza jana nje ya gereza hilo, wafuasi hao walisema walipofika hapo saa nne asubuhi waliambiwa kwamba tayari ndugu zake wanne walikwisharuhusiwa kuingia kumwona.
“Tumeambiwa kwamba idadi watu hao inatosha na kwamba wengine haturuhusiwi kumwona,” alisema mmoja wa wafuasi hao, Baraka Mohamed na kuongeza: “Tunaendelea kusubiri huruma za askari wa Magereza labda baadaye wanaweza kuturuhusu kumwona,” alisema.
Wafuasi hao ambao walijaza sehemu kubwa ya eneo la mapokezi na nje ya gereza hilo walilalamikia kitendo cha askari hao kutokuwaruhusu kumwona kiongozi wao.
“Nimefika hapa asubuhi na mapema, lakini utaratibu sikuupenda kwa kweli. Nimezuiwa nami nataka kumwona kiongozi wangu na si mimi tu tuko wengi hapa,” alisema mfuasi huyo.
Wafuasi hao hawakukata tamaa kwani licha ya kuzuiwa waliamua kukaa jirani na lango la gereza na wengine kusimama vikundi vikundi wakijadiliana namna ya kupata nafasi ya kumwona. Sheikh Ponda ambaye alikuwa amelazwa katika Taasisi ya Tiba na Mifupa Muhimbili (Moi) alipelekwa katika gereza hilo Alhamisi iliyopita.
Hatua hiyo ilikuja baada ya kusomewa shtaka la uchochezi akiwa kitandani akidaiwa kutenda kosa hilo katika maeneo mbalimbali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kati ya Juni 2 hadi Agosti 11 mwaka huu.
Kwa nini walizuiwa?
Ofisa Habari wa Jeshi la Magereza, Deodatus Kizinja alisema jana kuwa kisheria ni watu wawili katika kipindi cha wiki nne wanaoruhusiwa kumwona kila mahabusu.
Hata hivyo, alisema kwa kuzingatia sababu mbalimbali ambazo zimekuwa zikitolewa na wananchi, wamekuwa wakiruhusu idadi zaidi kila inapobidi.
“Kwa watu maarufu kama Ponda, Jeshi la Magereza linakuwa makini kudhibiti umati wa watu wanaotaka kumwona mahabusu kwa sababu hatuwezi kufahamu kama watu wote wana nia njema au la,” alisema Kizinja na kusisitiza kuwa ndugu zake wanne ambao walishaingia kumwona wanatosha.

No comments:

Post a Comment